Saturday, January 7, 2012

Chekelea Time!!

Baada ya kushehereka na Sikukuu ya krismasi na kuukaribisha mwaka 2012 Kidarubini kimekuja na Chekelea Time itakayokuwa inawajia mtandaoni kwa njia ya kushtukiza kwee kwee kwee!!Leo somo la Chit-Chat linahusu methali ambazo wengi wetu tutakuwa tunazikumbuka vizuri.
Mwalimu: Simameni!
Wanafunzi: Shikamoo mwaaaa--limu.
Mwalimu: Kaeni.
Wanafunzi: Asante mwaaaa--limu.
Mwalimu: Haya, leo ninataka nijue nani anazikumbuka methali tulizojifunza jana. Mwenye kufahamu anyooshe kidole juu. Penye kuku wengi...?
Kipensi ananyoosha kidole.
Mwalimu: Kipensi, malizia methali.
Kipensi: Penye kuku wengi chagua mmoja awe kitoweo!
Mwalimu: Mh!!! Haya, methali ya pili. Mtoto akililia wembe...?
Kisistimu ananyoosha kidole.
Mwalimu: Haya Kisistimu malizia methali.
Kisistimu: Mtoto akililia wembe atakuwa kinyozi!
Mwalimu: Duh! Haya tuendelee. Asiyesikia la mkuu...?
Kiroba ananyoosha kidole.
Mwalimu: Haya Kiroba, malizia methali.
Kiroba: Asiyesikia la mkuu, itakuwa sio mwanae wala hawana uhusiano!
Mwalimu: Nauliza methali ya mwisho, sitaki jibu la ovyo vinginevyo nitawapatia adhabu darasa zima. Mbio za sakafuni...?
Kipensi ananyoosha kidole.Mwalimu: Haya Kipensi jibu.
Kipensi: Mbio za sakafuni, hazimo hata kwenye olimpiki!!
Mwalimu: Dah!! Acha tu nirudi kijijini nikalime.

No comments:

Post a Comment